Kilio cha Boda boda
Habari za kuzubaa, nyie
mlio vitini,
Taratabu twatambaa,
tukijia mlikoni,
Katu hatutabung’aa,
tuishie kafarani,
Tuk-tuk zimwi kweli,
limetumwagia unga,
Limetumwagia unga, na
kutubwaga njaani,
Taratibu tunakonga, jamaa
tulishieni,
Sie twaliita janga, bora
katuloleeni,
Tuk-tuk zimwi kweli,
limetumwagia unga,
Kheri lende majijini,
litoke huku shambani,
Sasa kazi hatuoni,
bukrata ashiyani,
Ushuru tulipieni, kiwa
pato hatuoni,
Tuk-tuk zimwi kweli,
limetumwagia unga,
Sio siri tunalia, hasa
huku Magharibi,
Katu hatutatulia, twaja
hata Nairobi,
Tutaja jiamulia, kipuza
yetu maombi,
Tuk-tuk zimwi kweli,
limetumwagia unga,
Japo ni njia ya pato, ni
uhaini mkuu,
Ni kipato cha mkato, kwa
idadi iso kuu,
Ndo twasihi Kiroboto,
awasilishe kukuu,
Tuk-tuk zimwi kweli,
limetumwagia unga,
Kwa ufupi viongozi, shoti
tendeni khisani,
Tuondolee vigunzi,
twendelee kwa amani,
Litende jijini kazi,
lituachie shambani,
Tuk-tuk zimwi kweli,
limetumwagia unga.
Hapa Kiroboto nilikuwa nawatetea wahudumu wa Boda Boda dhidi ya mjo wa tuk-tuk. Haa, nalo lilichapishwa kwenye Taifa Leo na kulumbwa na wengi hususan Malenga Wa Kijiweni, Abubakari Rajabu wa pale Steji Mjini mumias. Ni mwendeshaji Tuk Tuk na hivyo basi sikubungaa kuona akikinza! Ni rafiki yangu na asili ya lakabu yangu. nampenda! Mgalla umwuuwapo haki mpe jamani!!!