Friday 11 May 2012


Kilio cha Boda boda

Habari za kuzubaa, nyie mlio vitini,
Taratabu twatambaa, tukijia mlikoni,
Katu hatutabung’aa, tuishie kafarani,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Limetumwagia unga, na kutubwaga njaani,
Taratibu tunakonga, jamaa tulishieni,
Sie twaliita janga, bora katuloleeni,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Kheri lende majijini, litoke huku shambani,
Sasa kazi hatuoni, bukrata ashiyani,
Ushuru tulipieni, kiwa pato hatuoni,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Sio siri tunalia, hasa huku Magharibi,
Katu hatutatulia, twaja hata Nairobi,
Tutaja jiamulia, kipuza yetu maombi,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Japo ni njia ya pato, ni uhaini mkuu,
Ni kipato cha mkato, kwa idadi iso kuu,
Ndo twasihi Kiroboto, awasilishe kukuu,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Kwa ufupi viongozi, shoti tendeni khisani,
Tuondolee vigunzi, twendelee kwa amani,
Litende jijini kazi, lituachie shambani,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga.

Hapa Kiroboto nilikuwa nawatetea wahudumu wa Boda Boda dhidi ya mjo wa tuk-tuk. Haa, nalo lilichapishwa kwenye Taifa Leo na kulumbwa na wengi hususan Malenga Wa Kijiweni, Abubakari Rajabu wa pale Steji Mjini mumias. Ni mwendeshaji Tuk Tuk na hivyo basi sikubungaa kuona akikinza! Ni rafiki yangu na asili ya lakabu yangu. nampenda! Mgalla umwuuwapo haki mpe jamani!!!
 

No comments:

Post a Comment