Wednesday 9 May 2012


Mnara wa walotuuka

Mwaambaje mashabiki, mpendao penye haki,
Mnopenda kudhihaki, mipigo ya kimziki,
Leo ninawahakiki, nitawapa yangu jeki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Sisemi ninadhihaki, miye ni kindakindaki,
Pia naipenda haki, na mwenye chuki kwa chuki,
Iwapo meinywa siki, mwambe nitie breki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Ikiwepo taharuki, hiyo yangu mabruki,
Bora nipige mswaki, kinywa kisizue chuki,
Nilipolenga mkuki, ni pa Kiswahili hiki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Nimeumwa kwa mawiki, kwa walosema ashiki,
Semi hazirekebiki, na mithali mahuluki,
Sasa swali washiriki, nijibu kimantiki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Mbona haurekebiki, mnara uso wa haki,
Sarufi haitiiki, bado mwasema si baki,
Ama mbovu mwadiriki, sumu hamnusuriki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Wengi wenu nahakiki, mmejitanda kaniki,
Mwatafuta na mikuki, m’ue Kiroboto hiki,
Ila mie sitishiki, kwani haizami haki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Nikiaga mashabiki, salamani mkabaki,
Mbakiapo rafiki, Mola na awabariki,
Nodhani ni unafiki, kishairi dai haki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Maelezo: Shairi hili nililitunga mwaka 2007 wakati ambapo mabadiliko mengi yalikuwa yakifanyiwa lugha ya Kiswahili hususan yakiongozwa na mwalimu Wallah Bin Wallah. Japo simpingi mwaliumu Yule, yapo mengi ambayo sikubaliani nayo kulingana na shairi langu hilo.

No comments:

Post a Comment