Wednesday 9 May 2012

Fundo chunga la Moyoni

Ewe unosoma lino, niwe mie nakujia,
Nakunyoshea mikono, magoti nakupigia,
Uneleze ya uono, ya wengi kuwachukia,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Mbona wayatoa macho, mithili ya bundi kaka,
Na pia kisucho hicho, alani mbona siweke,
Eti mabezo kitocho, daima kasawijika,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Kila mara kiniona, watamani kunifyanda,
Hata tunapokutana, kusalimu hutapenda,
Japo ni wa kwenu mwana, unapanga kuniponda,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Ama kweli u zandiki, kanisani u shabiki,
Wajitia kushiriki, kutekeleza hutaki,
Maadaili wadhihaki, hata bora sishiriki,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Iwapo mie tajiri, huji nikakupe siri,
Wapangia usihiri, wapanga kunihasiri,
Mwisho utie kaburi, kidhani metenda heri,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Kwa ufupi ndugu zangu, tuasi yetu khiana,
Tusoneane machungu, ili tuweze kupona,
Chunga tusichushe Mungu, kwa daima kukinzana,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Maelezo: Shairi hili nililitunga mwaka 2007 . Nilikuwa katika harakati za kujiunga na chuo kikuuu. Pia ni wakati huu ambapo mashairi yangu yalikuwa yakivuma mno katika gazeti la Taifa Leo. Si wengi waliokuwa wakifurahishwa na maendeleo yale. Ndiposa nikawasihi wayafundukhule mafundo nyoyoni kwani kila mja na nyota yake!!

No comments:

Post a Comment