Tuesday 18 September 2012

Wanga wawa dume gani?!

Eddi nipelo sikizi, Mpole nasema nawe,
Umegeuka kilizi, sababu nomba nijuwe,
Una nini siku hizi, tuambie tukijuwe,
Wanga wawa dume gani, kulialia ja mwana.

Kulialia ja mwana, redioni gazetini,
Kifo nani hataona, ndo kijaze mdomoni,
Unawapotosha wana, toa mfano mwanani,
Wanga wawa dume gani, Mpole nakushangaa.

Mpole nakushangaa, malenga wa Visramu,
Kijua umekomaa, kumbe bado kuhitimu,
Ni bora ukinyamaa, usidhaniwe wazimu,
Wanga wawa dume gani, nahurumia mkeo.

Nahurumia mkeo, kwani kulea hakomi,
Hamna aso upeo, acha kuzitoa kemi,
Hujui kifo ni cheo, sio cha mapeni kumi,
Wanga wawa dume gani, wawasiwasika bure.

Wawasiwasika bure, hakuna anokwandama,
Zikumbuke hamrere, kwa wengi ulizotuma,
Ndizo zafanya uhare, pole hutaki kusema,
Wanga wawa dume gani, wanishangaza Mpole,

Wanishangaza Mpole, mie mkongwe bondeni,
Wazileta siku zile, Kizere kivuma ndani,
Uje kwangu tuselele, juma zima mafunzoni,
Wanga wawa dume gani, kulia achia wana.

Chombo kikitia nanga


Mzee ni ukumbini, na tabu la ujanani,
Natia macho miwani, nimsomee Fulani,
Maisha ya duniani, wangi hawajui nini,
Chombo kikitia nanga, si mwisho wa usafiri.

Si mwisho wa usafiri, hata kama umefika,
Huishi kwenye bandari, kwenda zaidi tataka,
Ipe mgongo bahari, na uikabili njia,
Chombo kikitia nanga, teremka kwa makini.

Teremka kwa makini, uikague sehemu,
Jua lengo kuu nini, nakili kwa tarakimu,
Kama ndipo ubaini, lau sipo ufahamu,
Chombo kikitia nanga, yasubiri maelezo.

Yasubiri maelezo, usanze bure kuranda,
Yako kote matatizo, kokote unakokwenda,
Hayakeri maulizo, wangi mno mewalinda,
Chombo kikitia nanga, usanze kutoa mali.

Usanze kutoa mali, itatwaliwa haraka,
Ufikiri mara mbili, uhakiki umefika,
Wanolipuuza hili, huchekwa wanapotoka,
Chombo kkitia nanga, sikiza yao wazee.

Sikiza yao wazee, kama miye Kimpole,
Tukiteswa tutetee, radhi tulinazo tele,
Acha nende waombee, Mola awone milele,
Chombo kikitia nanga, umkumbuke Rabuka.

Tuesday 17 July 2012

Mbogholi akoga

Mbogholi ni malaika?!

Mkwiro naukamata, kigoma nanzekipiga,
Mati natakaziita, zone Mbogoli kikoga,
Huyu mtoka Taveta, uungu akauiga,
Mbogholi ni Malaika, waja awona shetani.

Waja awona shetani, hasa wale wa siasa,
Amewatia doani, eti ni hakimu sasa,
Natakajua ni nani, Ludo amemtakasa,
Mbogholi ni Malaika, adharau viongozi.

Adharau viongozi, akawaita mikia,
Eti kikaza maozi, awaona masinia,
Naona akosa kazi, wengine kawangilia,
Mbogholi ni Malaika, wasoye mauzauza.

Wasoye mauzauza, wanasiasa asema,

Awaita walooza, kwa makali awachoma,

Kwamba wanajidekeza, wote atakawatema,
Mbogholi ni Malaika, ndiye aliyetimia.

Ndiye aliyetimia, kama siasa ajua,
Nani amemuambia, kina suluhu kifua,
Mpole namuusia, pae kijuwa kutua,
Mbogholi ni Malaika, kesho aende mbinguni.

Kesho aende mbinguni, kusiko hawa majibwa,
Ajuwe hayezekani, dunia iso na chapwa,
Siasa daima duni, ni kunguru alorembwa,
Mbogholi ni Malaika, Mpole namshangaa!

SYLVESTER OCHIENG
AlmaarufuKiroboto Mpole
Kituo cha Lugha za Ughaibuni,
Eldoret.

Tungo Mseto


Toloi kupata wana

Mpole ninaingia, na hongera chekwachekwa,
Nampongeza Rukia, Waluhya tunamjuwa,
Mola amemjibia, kwani wana amepewa,
Toloi kupata wana, ni ishara yake Mungu.

Ni ishara yake Mungu, Bwana wa wokovu wetu,
Tumpe yetu machungu, anaweza vyote vitu,
Mwenye dunia na mbingu, alomkumbuka Lutu,
Toloi kupata wana, kuimarishe imani.

Kuimarishe imani, kati yetu waumini,
Tutambue Mungu nani, tudumu kumuamini,
Siyumbeyumbe jamani, wala simjaribuni,
Toloi kupata wana, kweli ni mwamko mpya.

Kweli ni mwamko mpya, tulioupata waja,
Liwe ni fundisho Kenya, kuwa maombi daraja,
Bwana Mungu wa Eliya, tatupa tukimngoja,
Toloi kupata wana, ni furaha kwetu sote.

Ni furaha kwetu sote, tunamtukuza Mola,
Mungu Muweza wa yote, asante kujibu sala,
Tuzuie tusikwate, wewe huna kibadala,
Toloi kupata wana, ni hidaya kubwa hino,

Ni hidaya kubwa hino, Kiroboto naswifia,
Namwinua Mungu mno, tena namsujudia,
Katimizia maono, wale nilohurumia,
Toloi kupata wana, la ziada sina tena.

La ziada sina tena, ila nasaha hatima,
Toloi leeni wana, kwa ndia iliyo njema,
Wakamheshimu Bwana, isiwapate nakama,
Toloi kupata wana, shangwe Mulembe Ef Emu.

Ochieng’ O. Sylvester
Kiroboto Mpole”
Chuo Kikuu Cha Moi
Chepkoilel.






Kwaheri Mrono

Mpole nina kilio, kilio cha Kiswahili,
Silipati kimbilio, kulitia pigo hi9li,
Mauti faradhi ndio, bali hiki kikatili,
Kwaheri ndugu Mrono, mwalimu wa heba kubwa.

Twamshukuru Rabuka, kwa maishayo mwandani,
Sie tutakukumbuka, kwa kaziyo vitabuni,
Kukupeza ni hakika, sautiyo redioni,
Kwaheri ndugu Mrono, mwalimu wa heba kubwa.

Wapenzi wa Kiswahili, tumebaki vinywa wazi,
Kote metulia tuli, tangu lizame jahazi,
Mwenzetu kwa kwenda mbali, umetutia duwazi,
Kwaheri ndugu Mrono, mwalimu wa heba kubwa.

Bahari yetu si shwari, imechafuka watani,
Tangu uwe mhajiri, hatwoni chako kifani,
Twafazaika twakiri, hatutaki kuamini,
Kwaheri ndugu Mrono, mwalimu wa heba kubwa.

Kaketu wende salama, mikono yetu twapunga,
Wasalimie wa zama, akina Mwalimu Mbega,
Twakwombea kwa Karima, na dhiki atakutenga,
Kwaheri ndugu Mrono, mwalimu wa heba kubwa.

Kituoni nikifika, rambirambi nazituma,
Makiwa ndu’ watukuka, nayo familia nzima,
Haya mambo ya Rabuka, nayo mauko lazima,
Kwaheri ndugu Mrono, mwalimu wa heba kubwa.

Ochieng’ O. Sylvester
Kiroboto Mpole”
Chuo Kikuu Cha Moi
Chepkoilel.



Saturday 7 July 2012

Wangu lia shambani

Mpole nimeghasiwa, na waibaji wa miwa,
Nawamiminia dawa, sina shaka wauguwa,
Taksiri niwatowa, si kwa nia kuumbuwa,
Wangu ulie shambani, sondoke nao kiumbe.

Ungaingia shambani, una uhuru mwandani,
Chaguwa pahala ndani, utapotulia chini,
Hata kama mafichoni, sijali sitokuhini,
Wangu ulie shambani, sondoke nao kiumbe.

Uubambue maganda, ubakiye utakavyo,
Utende utavyotenda, upate wako mchovyo,
Kama mcheza kandanda, shinda jinsi uwezavyo,
Wangu ulie shambani, sondoke nao kiumbe.

Tafuna kisha unyonye, utamu saizi yako,
Mie nani nikukanye, shambani sina uchoko,
Maliza chafu usanye, na uende uendako,
Wangu ulie shambani, sondoke nao kiumbe.

Lakini nakwonya wewe, mzoea kugurisha,
Ya kwangu usiondowe, ukangia kuharisha,
La sivyo nikuripuwe, kufisha nitakufisha,
Wangu ulie shambani, sondoke nao kiumbe.

Kabula nitie tuo, mwenye kono ujitenge,
Nikupa langu funguo, na mwako pia sifunge,
Nikija nile chaguo, lolote usinipinge,
Wangu ulie shambani, sondoke nao kiumbe.

Utunzi wa: Malenga Kimpole,
Eldoret (K).

Wednesday 6 June 2012

                                                                                                           Leo, Juni  2012
Nisamehe

Mpole sina afia, sina nguvu za mwilini,
Kama mtoto nalia, nina uchungu moyoni,
Kujuta ninajutia, nimekuudhi fulani,
Dada nipe msamaha, ili nipate amani.

Nashukuru sikufuru, Mola asinadhibu,
Ingawa nilikudhuru, najua utanitibu,
Kwako nitapata nuru, nikisogea karibu,
Dada nipe msamaha, ili nipate amani.

Ili niwe na amani, msamaha ni muhimu,
Siwa mkosa imani, najua kuna hukumu,
Nahofu moto jamani, nisamehe nihitimu,
Dada nipe msamaha, ili nipate amani.

Uandishi kazi yangu, dada haina mipaka,
Nawafaa wa kiungu, nao waliopotoka,
Napoza wenye uchungu, nachafua wanotaka,
Dada nipe msamaha, ili nipate amani.

Donge nililokupa, kumbe si saizi yako,
Nashukuru ulitupa, lingenyonga koo lako,
Kama nyama ya mfupa, bila meno ni unoko,
Dada nipe msamaha, ili nipate amani.

Hatimaye nakuaga, ni mwishoni mwa shairi,
Nenda bafuni kukoga, unitoke uhinziri,
Sitaki tena kuzuga, sio mzuri ushari,
Achieng’ nisamehe, ili nipate amani.

Wasalaam.
Malenga Kiroboto Mpole, (Kimpole)
Itigo, Eldoret.



Friday 11 May 2012


Kilio cha Boda boda

Habari za kuzubaa, nyie mlio vitini,
Taratabu twatambaa, tukijia mlikoni,
Katu hatutabung’aa, tuishie kafarani,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Limetumwagia unga, na kutubwaga njaani,
Taratibu tunakonga, jamaa tulishieni,
Sie twaliita janga, bora katuloleeni,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Kheri lende majijini, litoke huku shambani,
Sasa kazi hatuoni, bukrata ashiyani,
Ushuru tulipieni, kiwa pato hatuoni,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Sio siri tunalia, hasa huku Magharibi,
Katu hatutatulia, twaja hata Nairobi,
Tutaja jiamulia, kipuza yetu maombi,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Japo ni njia ya pato, ni uhaini mkuu,
Ni kipato cha mkato, kwa idadi iso kuu,
Ndo twasihi Kiroboto, awasilishe kukuu,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga,

Kwa ufupi viongozi, shoti tendeni khisani,
Tuondolee vigunzi, twendelee kwa amani,
Litende jijini kazi, lituachie shambani,
Tuk-tuk zimwi kweli, limetumwagia unga.

Hapa Kiroboto nilikuwa nawatetea wahudumu wa Boda Boda dhidi ya mjo wa tuk-tuk. Haa, nalo lilichapishwa kwenye Taifa Leo na kulumbwa na wengi hususan Malenga Wa Kijiweni, Abubakari Rajabu wa pale Steji Mjini mumias. Ni mwendeshaji Tuk Tuk na hivyo basi sikubungaa kuona akikinza! Ni rafiki yangu na asili ya lakabu yangu. nampenda! Mgalla umwuuwapo haki mpe jamani!!!
 

Wednesday 9 May 2012

Fundo chunga la Moyoni

Ewe unosoma lino, niwe mie nakujia,
Nakunyoshea mikono, magoti nakupigia,
Uneleze ya uono, ya wengi kuwachukia,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Mbona wayatoa macho, mithili ya bundi kaka,
Na pia kisucho hicho, alani mbona siweke,
Eti mabezo kitocho, daima kasawijika,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Kila mara kiniona, watamani kunifyanda,
Hata tunapokutana, kusalimu hutapenda,
Japo ni wa kwenu mwana, unapanga kuniponda,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Ama kweli u zandiki, kanisani u shabiki,
Wajitia kushiriki, kutekeleza hutaki,
Maadaili wadhihaki, hata bora sishiriki,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Iwapo mie tajiri, huji nikakupe siri,
Wapangia usihiri, wapanga kunihasiri,
Mwisho utie kaburi, kidhani metenda heri,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Kwa ufupi ndugu zangu, tuasi yetu khiana,
Tusoneane machungu, ili tuweze kupona,
Chunga tusichushe Mungu, kwa daima kukinzana,
Fundo chungu la moyoni, linakufaidi nini.

Maelezo: Shairi hili nililitunga mwaka 2007 . Nilikuwa katika harakati za kujiunga na chuo kikuuu. Pia ni wakati huu ambapo mashairi yangu yalikuwa yakivuma mno katika gazeti la Taifa Leo. Si wengi waliokuwa wakifurahishwa na maendeleo yale. Ndiposa nikawasihi wayafundukhule mafundo nyoyoni kwani kila mja na nyota yake!!

Mnara wa walotuuka

Mwaambaje mashabiki, mpendao penye haki,
Mnopenda kudhihaki, mipigo ya kimziki,
Leo ninawahakiki, nitawapa yangu jeki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Sisemi ninadhihaki, miye ni kindakindaki,
Pia naipenda haki, na mwenye chuki kwa chuki,
Iwapo meinywa siki, mwambe nitie breki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Ikiwepo taharuki, hiyo yangu mabruki,
Bora nipige mswaki, kinywa kisizue chuki,
Nilipolenga mkuki, ni pa Kiswahili hiki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Nimeumwa kwa mawiki, kwa walosema ashiki,
Semi hazirekebiki, na mithali mahuluki,
Sasa swali washiriki, nijibu kimantiki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Mbona haurekebiki, mnara uso wa haki,
Sarufi haitiiki, bado mwasema si baki,
Ama mbovu mwadiriki, sumu hamnusuriki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Wengi wenu nahakiki, mmejitanda kaniki,
Mwatafuta na mikuki, m’ue Kiroboto hiki,
Ila mie sitishiki, kwani haizami haki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Nikiaga mashabiki, salamani mkabaki,
Mbakiapo rafiki, Mola na awabariki,
Nodhani ni unafiki, kishairi dai haki,
Mnara wa lotuuka, mbona haurekebiki.

Maelezo: Shairi hili nililitunga mwaka 2007 wakati ambapo mabadiliko mengi yalikuwa yakifanyiwa lugha ya Kiswahili hususan yakiongozwa na mwalimu Wallah Bin Wallah. Japo simpingi mwaliumu Yule, yapo mengi ambayo sikubaliani nayo kulingana na shairi langu hilo.

Tuesday 8 May 2012

Karibuni wapenzi washairi

Karibuni
Hatimaye nimetua,
Paso jua wala mvua,
Si kwamba nilipajua,
Ni Mola mwenye kwamua.

Karibuni mpate tungo za kimpole, tungo zangu mie tangu nilipojibwaga utunzini. Mola mwema awabariki mnapozisoma nudumu za humu.